Waziri Kuria aitaka serikali kushughulikia maswala ya vijana kwa dharura

Dismas Otuke
1 Min Read

Waziri wa Utumishi wa Umma Moses Kuria amewataka viongozi serikalini kutopuuza matakwa ya Wakenya na badala yake kutafuta suluhu.

Kuria amesema wimbi la maandamano yaliyolikumba taifa siku chache zilizopita yanapaswa kuwa onyo kwa taasisi za serikali kwamba zinapaswa kukomesha ubadhirifu wa rasilimali za umma.

Akizungumza leo Alhamisi wakati wa uzinduzi wa mpango wa mkakati wa Shule ya Serikali Nchini, KSG wa mwaka 2023-2027, Kuria alisema hivi karibuni atawasilisha pendekezo kwa Baraza la Mawaziri lenye lengo la kuwashurutisha maafisa wa serikali miongoni mwa watu wengine kupewa mafunzo ya namna ya kuishi kulingana na uwezo wao wa kiuchumi.

Kuria alisisitiza haja ya kuhakikisha kodi inayokusanywa kutoka kwa Wakenya kwa ajili ya maendeleo nchini inatumiwa ipasavyo.

Matamshi yake yanakuja wakati Wakenya wamepinga vikali Mswada wa Fedha 2024 wakisema utasababisha wao kutozwa kodi zaidi wakati hali ya maisha tayari ni ngumu.

Kunao wanaolalamikia ubadhirifu wa rasilimali za umma, lalama ambayo Mwakilishi wa Wanawake wa kaunti ya Nairobi Esther Passaris anakubaliana nayo akisema kuwa taifa hili linaweza likapiga hatua kubwa kimaendeleo iwapo tu ufisadi utakomeshwa serikalini.

Website |  + posts
TAGGED:
Share This Article
Leave a Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *