Maafisa wa polisi wanawasaka wafanyakazi wawili wa kampuni ya ulinzi ya Wells Fargo ambao walitoweka na milioni 94 za duka la jumla la Quickmart ambazo walikuwa wakisafirisha kuelekea benki.
Wawili hao ambao wametambuliwa kama Daniel Mungai kamanda wa kikosi kidogo kilichojukumiwa kusafirisha pesa hizo na dereva Anthony Nduiki walitoweka leo asubuhi wakitumia gari aina ya Isuzu canter nambari ya usajili KBA 517T.
Inasemekana kwamba walikwenda kuchukua pesa hizo kama ilivyo kawaida lakini wakatoweka bila ulinzi kutoka kwa maafisa wa polisi kama ilivyo ada.
Polisi wa kitengo cha AP ambao walistahili kuandamana na wawili hao waliwasubiri lakini hawakutokea ndiposa wakafahamisha kampuni ya Wells Fargo.
Gari walilotumia linasemekana kuachwa mtaani South B, kaunti ndogo ya Lang’ata, kaunti ya Nairobi.