Kenya itaandaa Kongamano la Dunia la Shirikisho la Kimataifa la Walimu Wakuu, ICP mwezi Agosti mwaka huu.
Kongamano hilo litakaloandaliwa mjini Mombasa liatafanyika kati ya 19-23.
ICP ni shirikisho la dunia linalodhamiria kuendeleza, kusaidia na kuhamasisha uongozi wa shule duniani.
Jana Alhamisi, maafisa wa ICP wakiongozwa na Sofia Hughes ambaye ni Katibu Mkuu wake na Leendert-Jan Veldhuyzen ambaye ni Rais walikutana na Katibu katika Wizara ya Elimu Dkt. Belio Kipsang.
Waliandamana na mwenyekiti wa Chama cha Wakuu wa Shule za Sekondari, KESSHA Willy Kuria na mwenyekiti wa chama hicho anayeondoka Kahi Indumuli.
Dkt. Kipsang aliwahakikishia maafisa hao kwamba serikali itaunga mkono uandaaji wa kongamano hilo.
Kwa upande wake, Hughes alisema maudhui ya mkutano huo yatakuwa “Njia za Siku Zijazo za Mafunzo na Wanafunzi.”
Hughes aliipongeza Kenya kwa kupigania kuandaa kongamano hilo akisema nchi hii ina miundombinu inayohitajika kuandaa kongamano hilo.
ICP ni shirikisho la dunia la vyama vya uongozi wa shule ambalo wanachama wake wanatoka Afrika, Amerika, Asia na Oshenia, na Ulaya.