Muungano wa upinzani, Azimio One Kenya, umeishutumu serikali kwa kukodi majangili kuvuruga maandamano yao ya amani wiki hii.
Kinara wa walio wachache katika bunge la Taifa Opiyo Wandayi, amesema kuwa serikali imekuwa ikilitumia kundi haramu lililojihami kuvuruga maandamano ya upinzani kulalamikia gharama ya juu ya maisha.
Wandayi amedai njama ya kutumia wahuni kuvuruga maandamano yao imejadiliwa na kundi la wabunge wanaogemea upande wa serikali.
Muungano huo umesisitiza kuwa utaendelea na maandamano yao ya siku tatu wiki hii licha ya takriban watu 17 kufariki katika sehemu mbalimbali nchini kutokana na maandamano ya wiki jana.